Tuesday, August 3, 2010

Hotuba ya Matokeo Kura ya Maoni



HOTUBA YA JANUARY MAKAMBA BAADA YA KUTANGAZWA KWA MATOKEO YA KURA ZA MAONI YA UBUNGE JIMBO LA BUMBULI KWA TIKETI YA CCM ILIYOTOLEWA KATIKA UKUMBI WA OFISI YA CCM WILAYA YA LUSHOTO, JUMATATU TAREHE 2 AGOSTI, 2010 .

(Imeandikwa baada ya kuzungumzwa).

CCM Oyee! (Oyeee!)
CCM Oyee! (Oyeee!)
Bumbuli mpoo? (Tupoo!)

Nashukuru sana.

Sasa, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa rehema zake. Tupo tumefika hapa leo tulipo kwasababu ameamua iwe hivyo. Ametujalia uhai, uzima na afya kati yetu. Kwahiyo ni muhimu kumshukuru.

Pili, napenda kuwashukuru wazazi wangu kwa malezi mazuri, kwa mchango wao mkubwa kwenye maisha yangu mpaka nimefikia hapa nilipofikia leo. Pia familia yangu – mke wangu na wanangu wawili – bahati mbaya hawapo [hapa] – wamesafiri. Lakini nawashukuru kwa kunitunza, kwa kukubali kukabiliana na hizi presha za siasa, na kuniunga mkono na kuwa na mimi wakati wote.

Lakini vile vile namshukuru bosi wangu, Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Namshukuru kwa kunikubalia nimtoroke kidogo kazi na kuja kufanya huu mradi, na namshukuru kwa ushauri na malezi ya kisiasa aliyokuwa akinipa wakati wote.

Lakini sana sana, nawashukuru wana-CCM wa Bumbuli kwa kuniamini - kwa kuniamini kwa kiasi kikubwa namna hii kwa kunipa kura nyingi sana. Waswahili wanasema, “Imani huzaa imani”. Imani waliyonipa kwa kura wanizonipa ni kubwa sana. Tutasherehekea leo, lakini kesho tutakumbuka kwamba kura hizo ni…maana yake ni kwamba wanategemea mengi kutoka kwangu. Na mimi naahidi kwamba sitawaangusha. Nitaibeba bendera ya Chama chetu cha Mapinduzi, na kuipeperusha na kuinadi Ilani yetu kwa uwezo wangu wote, kwa maarifa yangu yote na vipaji vyangu vyote nilivyojaliwa na Mwenyezi Mungu. Na naamini kabisa kwamba Chama chetu kitapata mshindi mkubwa sana kwenye jimbo la Bumbuli.

Lakini pia ningependa kuwashukuru wenzangu - wagombea wenzangu tulioshiriki nao, kwa kuonyesha ustaarabu mkubwa. Tumevumiliana, tumeheshimiana kwenye mchakato mzima. Ndugu yangu Kaniki mmemuona mwenyewe ni kijana mzuri, amekomaa vizuri.

Mzee Shelukindo – naomba niseme machache kuhusu Mzee Shelukindo, bahati mbaya hayupo hapa. Lakini kuvunjika kwa koleo sio mwisho wa uhunzi. Leo wana-CCM wameamua… jana wameamua, kwamba mwingine apeperushe bendera ya Chama chao kwenye uchaguzi mkuu. Lakini heshma ya Mzee Shelukindo katika nchi yetu bado ipo pale pale (makofi). Kwa kushindwa kura hizi za maoni, haina maana kwamba heshima yake na rekodi yake ya utumishi imepotea kabisa. Hapana. Ni maamuzi ya wanachama. Binafsi nitaendelea kumuheshimu kama Mzee, lakini [pia] kama kiongozi wa muda mrefu kwenye Serikali. Ni hazina kubwa ya uzoefu kwenye jimbo letu, na bado ni mwanachama wa CCM. Na binafsi nitaenda kumuomba rasmi…hatujakutana tangu tumalize mchakato huu, lakini nitamtembelea nyumbani kwake kumuomba kwamba tusaidiane kikazi (makofi).

Lakini naomba niwashukuru wapiganaji wangu walionisaidia kunadi jina langu. Walionisaidia kuwashawishi wana-CCM wa Bumbuli kwamba mimi nafaa. Nawashukuru kwa kazi nzuri. Ushindi huu uliopatikana ni matunda ya kazi yenu. Lakini vile vile naomba niwaambie kwamba uchaguzi umekwisha jana. Mpambano umekwisha. Sasa hivi sote tunarudi kwenye hema la Chama chetu cha Mapinduzi. Sina uadui na Mzee Shelukindo. Sina uadui na Bwana Kaniki. Sina uadui na Mzee Mshihiri (makofi). Sina uadui na mtu yoyote aliyeshiriki kwenye mchakato huu.

Kwahiyo wapiganaji wangu, nawaomba sana sana sana tuache tambo. Tuache kutambiana. Uchaguzi umekwisha jana. Kazi ya kunipigania imeisha, tunaanza kazi ya kukipigania Chama chetu. Ndio kazi iliyo mbele yetu, na naomba tuifanye kwa umoja, tukishirikiana na wale ambao hawakuniunga mkono kwenye mchakato huu. Kwa nguvu ile ile ambayo mlinipigania mimi, naomba sasa nguvu hiyo muielekeze katika kukipigania Chama chetu kwenye uchaguzi mkuu wa mwezi Oktoba mwaka huu.

Naomba vile vile nitoe shukrani na pongezi zangu kwa uongozi wa Chama Wilaya, Katibu wa Wilaya na timu yake. Wilaya yetu ina majimbo matatu na kata 44. Zoezi hili ni zoezi kubwa, hasa kusimamia chaguzi za madiwani katika kata zote hizi. Ni kazi inayohitaji uwezo mkubwa, inahitaji rasilimani za uendeshaji na uwezo mkubwa wa kiutawala. Natambua kwamba zimejitokeza kasoro za hapa na pale, lakini naamini kwamba kasoro hizo zinatokana na upya wa mfumo wetu huu mzuri wa kurudisha demokrasia kwa wanachama kuchagua ni nani wawasimamishe kupeperusha bendera ya Chama kwenye uchaguzi wa wabunge na madiwani. Naamini kwamba matatizo yaliyojitokeza yatashughulikwa, na wakati ujao tutakuwa na utaratibu mzuri zaidi. Lakini vile vile naamini zaidi kwamba kasoro zilizojitokeza hazikumnyima mtu haki, na kwamba matokeo haya ya Bumbuli ni kielelezo halisi cha matakwa ya wanachama wa CCM wa Jimbo la Bumbuli.

Na mwisho, napenda kuwashukuru wote waliojitokeza hapa kunisikiliza, na nawatakia jioni njema. Nashukuru sana. (makofi)


January Makamba,
Agosti 2, 2010.

4 comments:

Azaria Mbughuni said...

Zumbe January Makamba, Washambalaa waghamba:“Hata mwelima he ubula wakwe aaghangwa nkonde tate.”

I want to congratulate you for the victory once again. The people of Bumbuli have spoken loud and clear. The victory was not an accident; it is the result of careful planning, diligence and foresight. Although the final election is not over yet, I believe this campaign will go in the annals of our nation’s history as one of the best for this generation. I hope it will signal the passing of the torch.

The acceptance speech is short and precise as it should be. It acknowledges all the people who have taken part in the elections and reminds us of the challenges ahead of us. This is just the beginning; the challenges ahead are enormous and the expectations are high, but I am confident that you will deliver on your promises.

Anonymous said...

http://vijana.fm/2010/08/04/january/

Anonymous said...

January,

Haya ni mashauri yangu machache ya kukujulisha.

1. Naomba ujitahidi ujaribu kudocument the whole process, hususan home video, notes and writings, ikijumuisha sauti za watu, sehemu unazopita, kwa kututupa historical background, iwe in a form ya documentary, kama time na pesa ipo ya kufanya hivyo. Sababu ya kusema hivi, pengine itasaidia watoto wetu in future to look up to true leadership, on which I have certain believe utakua hivyo.

na jengine kuondoa wabunge bogus kama hawa na kuwatia aibu waondoke kwenye bunge letu,

Ifuatayo ni profile ya aliyekua Mbunge wa Kinondoni, Idi Azan,

Amesoma salala Secondary School, ambayo haipo toka kipindi hicho, anachodai mwaka aliyosoma yeye 1980.

Jengine anadai amesoma University Computer Centre, there is no such thing in Tanzania , I doubt there is a Dar City College, on which he thought he attained his Diploma in 2004

Sijawahi kumuona mtu amesoma three different institute within 3 years attaining Diploma and two Certificate.

na huyu ni mmoja lakini wako wengi wa namna hii katika bunge letu, mimi sina shaka kwamba kuwa na elimu kubwa siyo tija ya kugombea ubunge, lakini a BLUNT lie kuwa mwanasiasa, I think that is treason.

Profile yake hii hapa toka bungeni,
http://www.parliament.go.tz/bunge/mpcv.php?vpkey=347
EDUCATIONS
School Name/Location Course/Degree/Award Start Date End Date Level
Magomeni Primary School Primary Education 1973 1979 PRIMARY
University Computer Centre Certificate in Computer Course 2003 2003 CERTIFICATE
Eastern& Southern African Mgt. Institute (ESAMI) Certificate 2003 2003 CERTIFICATE
Dar City College Diploma 2004 2005 DIPLOMA
Salalah Secondary School - Oman Secondary Education 1980 1982 SECONDARY
Institute of Adult Education - Dar es Salaam Secondary Education 2002 2003 SECONDARY

Anonymous said...

Mtu mzima, I am really encourage you have taken the right steps in documenting ushindi wako, ili ni certainly one of the aspects of the transparency on your quest for A GOOD LEADERSHIP, you have taken our advice seriously and intelligently, we are not in physical presence to help you out with your journey, but, we are with you in spirit, I have firm believe we have a common thinking and ideas going foward, although I must say, I dont like the way CCM political machine running the business right now.

I am certainly believing that, you are providing a POLITICAL CORRECTNESS on your quest for leadership. Thats the way to do it.

lakini mwambie Mzee wetu, baba yetu, Yusuf Makamba, achukue side step for now, particularly in politics, I reckon astaafu baada ya wewe kuchukua ubunge au baada ya awamu hii, lazima apasishe torch kwako. I am sure he will provide you with good advice for foreseable future.